EPUKA UCHOKORAA,MLEE HIVI MWANAO - waleo blog

Breaking

Sunday 2 February 2020

EPUKA UCHOKORAA,MLEE HIVI MWANAO


#MALEZI BORA   

UKUAJI BORA WA MWANAO:
 Cheza na zungumza naye; maendeleo ya mtoto wako huanza toka wakati wa mimba na hufanyika kwa haraka sana katika miaka michache ya mwanzo ya maisha ya mtoto. Unaweza kufanya mengi kuchochea maendeleo ya afya ya mtoto wako katika miaka hiyo ya mwanzo. Hiki ni kipindi ambacho unaweza mjengea mwanao ujuzi ambao ni msingi muhimu kwa maisha yake yote ya baadaye. Mwanao anakusikia na kujenga hisia akiwa tumboni. Gusa tumbo lako kwa upendo, msemeshe na mwimbie mwanao ili aanze kutambua sauti yako na kujenga upendo. Mwenzi wako pia anaweza kushika tumbo lako na kuongea na mwanae.


AMEZALIWA
  Mtoto wako kwa sasa anaona na kusikia, mtazame machoni ukiwa unatabasamu, ongea naye kwa kumwita jina lake, ongea na mwimbie kwa upole ili kujenga mahusiano naye. Hii inaweza kufanyika wakati unamnyonyesha, mwogesha mtoto, unambembeleza au wakati mwingine wowote unampomshika mtoto.


UTAMBUZI
Mtoto wako anavutiwa na vitu vyenye rangi mbalimbali, muonyeshe vitu vya rangi mbalimbali ili aweze kukuza uwezo wake wa kuona. Waweza tumia nguo zenye rangi mfano ‘kanga’ kupitisha kwenye macho ya mtoto.
Mwanao anapenda kuchezea mikono na miguu yake, mlaze kwenye mkeka au kitanda ili acheze kwa uhuru na kujenga misuli yake. Mguse au mmasaji mwanao kwa upole huku ukimwimbia.

ISHARA
Mtoto wako hulia kukuelezea mahitaji yake kama vile kunyonya, amejisaidia, anahisi joto. Jifunze kutambua mahitaji hayo ili kuyatekeleza ipasavyo na kwa wakati. Usijali kuhusu kuwa utamharibu mtoto wako kwa kumdekeza. Malezi chanya yatasaidia kujenga mahusiano bora ya mwanao na pia kujiamini. Mwanao anaanza kulala na tumbo na kugeuka na kufikia vitu vilivyowekwa karibu. Msogezee vitu vyenye rangi ya kung’ara na sauti ili kumsaidia kushika na kuimarisha misuli. Unaweza kutumia chekeche iliyotengenezwa, mpira mlaini na mwepesi au mwiko mdogo wa mbao. Mwanao anapendelea kuweka vitu mdomoni. Mpatie mwanao vitu visafi, visivyo na ncha kali au vidogo kama punje ili kuepusha kumkaba au maradhi.

KUONGEA
Mtoto wako anaweza kutoa sauti ya kujirudia rudia kwa mfano ‘ba ba ba’, ‘da da da’ au ‘ma ma ma’. Ongea naye kwa maneno kamili mfano ‘mama’ ‘baba’ ili kumrahisishia kujifunza lugha. Pia mtajie mwanao vitu unavyoona, sikia au nusa kwenye mazingira ya nyumbani. Mfano, ‘Mtazame baba yako/mama yako’ ‘Umemuona ng’ombe?’ Tumia sura na sauti yako kuonyesha hisia.


NAKILI
Mtoto wako anazidi kutambua sura yako, akikuona huruka ruka na kutabasamu kwa furaha, onesha upendo kwa kutabasamu, kucheka, kumsemesha na kumbeba ili kuimarisha mahusiano na upendo. Mtoto anaanza kuzoea utaratibu wa kila siku unaomfanyia mfano muda wa kuoga, kujisaidia na kulala. Msaidie kufuata utaratibu huo mfano kufuata muda wa kulala, kuoga nk ili kumjenga kimwili na kiakili. Mtoto hujihisi salama anapokuwa na mzazi au mlezi. Unapoondoka muage kwa upendo, kwa kumbusu, kumpungia mkono na mhakikishie kuwa utarudi ili kumjengea uwezo wa kujiamini na kutokuwa na hofu.
Mtoto anaanza kuinuka, kukaa na kutambaa na pia uwezo wa utambuzi unaongezeka. Mpatie vitu vya kuchezea vyenye maumbo, rangi na sauti tofauti tofauti ili aendelee kukua kiakili na kimwili. Mfano chupa tupu za maji zilizowekwa mawe madogo ili kutoa sauti, sufuria ndogo na mwiko ili kugonga nk. Ni muhimu kuhakikisha vifaa anavyopewa mtoto na mazingira ni safi na salama ili kumwepusha mwanao na hatari. Muweke mwanao mbali na moto au vitu vya moto, kamba, dawa au mafuta ya taa. Muweke mwanao mbali na maji yenye kina mfano kisima, bwawa au ndoo.


KAZI NDOGO NDOGO NA NYEPESI KABISA
Mtoto wako anaweza kujifunza, mpe vitu anavyoweza kupanga au kuingiza ndani ya vingine, mfano mikebe na vikombe; mruhusu akusaidie kupanga vitu, kama vile vibanio, soksi kwa jozi au rangi, pia anaweza kuchora kutumia kalamu na karatasi ili kumjengea misingi ya kujifunza. Mtoto wako anahitaji vitu vya kuchezea, sio lazima vinunuliwe, unaweza kutengeneza mwenyewe kwa kutumia vifaa vinavyopatikana kwenye mazingira yanayokuzunguka. Unaweza tengeneza mpira kutumia vitambaa vya nguo, kamba au majani ya mgomba, unaweza tengeneza mdoli kutumia nguo au majani ya mnazi. Mtoto wako anaweza kujifunza. Imba naye nyimbo za vitendo kama vile “simama kaa”, “ruka ruka”, au nyimbo za viungo vya mwili mfano ‘kichwa, mabega, magoti’ huku akionyesha viungo vyake ili kuendelea kumjengea misingi ya kujifunza zaidi. Mpongeze mwanao kwa vitendo anavyofanya. Mtoto wako anaweza kusimama, kutembea kwa kushika vitu/watu au mwenyewe. Mpatie vifaa mfano baiskeli ya mbao ya kusukuma ili kumjengea uwezo zaidi. Pia unaweza kutandika mkeka ili mtoto akianguka asiumie wakati anajaribu kutembea. Mpongeze mwanao kwa kumpigia makofi na kumwimbia.
Mtoto wako ana uwezo wa kusikiliza na kushika maneno machache, msimulie hadithi fupi, ili kumpa uwezo wa kufikiria na kuhifadhi kumbukumbu ya maneno. Waweza kumsimulia mwanao hadithi fupi au kusomea kitabu cha hadithi au picha. Pia unaweza kumwambia mwanao akuambie hadithi yake au tukio lotote analokumbuka, sikiliza ukitambua kuwa anaweza asiseme hadithi yote kwa makini na mpongeze. Mtoto wako anatambua rangi na vitu mbalimbali, mtengenezee picha na vitu mbalimbali kulingana na mazingira yenu mfano gari kutumia boksi au mdoli kutumia nguo na muelekeze kuvitambua, kulinganisha na kutofautisha mfano vifaa vikubwa na vidogo. Mtoto wako anaweza kuongea sentensi fupi yenye maneno mawili mpaka matatu, msaidie ayatamke vizuri na kujua maana yake ili aweze kujieleza vizuri.
Mtoto wako anapenda na anaweza kufanya vitu mwenyewe muelekeze afanye kwa usahihi, mfano kula chakula na kuvaa nguo ili aweze kujitegemea. Pia mtoto wako anapenda kusaidia kazi ndogondogo za nyumbani mfano, kufagia, kupanga vyakula toka sokoni na nguo zilizofuliwa mpongeze na muelekeze ili kumpa moyo wa kuendelea kujifunza.

BALEHE NA KUENDELEA
Wakati mtoto wako ana hamu ya kujitegemea, pia katika umri huu mtoto anaweza kukasirika kirahisi pale mambo yasipoenda sawa. Mfundishe mwanao aweze kufanya matendo mazuri kwa kumpa upendo, kumwelesha kuhusu taratibu na kanuni za nyumbani. Mpe mwanao upendo zaidi ya adhabu au kumgombeza. Kumkumbatia, kumbusu na kucheza naye kutadhibitisha upendo kwa mwanao. Kumpongeza na kumfuatilia mwanao kutamshawishi mwanao kufuata taratibu na kanuni zaidi ya kumpa adhabu. Mwanao anaongeza udadisi na kujifunza kwa kuuliza maswali mara kwa mara. Mjibu mwanao maswali yake kwa kumpa maelezo kwa kifupi.

Bakora na kumfokea kwa makosa atakayoyarudia itapendeza zaidi.
Share,comment,like ili wengine wakumbuke na waelimike.

No comments:

Post a Comment

Pages