UGONJWA WA TEZI DUME/BUSHA - waleo blog

Breaking

Wednesday 19 February 2020

UGONJWA WA TEZI DUME/BUSHA


 #AFYA

Tahadhari,makala hii imetumia picha za moja kwa moja bila kuficha kwa lengo la kufumbuana.

Tezi dume ni sehemu mojawapo ya mfumo wa uzazi wa kiume. Inaundwa na sehemu mbili, lobes, ambazo zimeunganishwa na kufunikwa kwa nje kwa utando wa tishu. Tezi hii ipo mbele kidogo ya puru (rectum) na na chini kidogo ya kibofu cha mkojo. Tezi dume inauzunguka mrija unaounganisha kibofu cha mkojo na uume (urethra).
Tezi dume ina sifa zifuatazo.
·             Ina umbo kama yai
·           Ina ukubwa wenye vipimo hivi, upana 4cm na unene 3cm ingawaje hivi vipimo vinatofautiana kwa kila mwanaume.
·           Tezi hii hua yenye ukubwa wa kawaida lakini huongezeka ukubwa kadri ya umri unavoongezeka.
·           Tezi hii hutengeneza majimaji yenye rutuba ya mbegu za kiume(shahawa) yanayochanganyika na mbegu za kiume (sperms) wakati wa kilele cha tendo la ngono. Mchanganyiko huu wa mbegu pamoja na majimaji hayo hufanya shahawa (semen). Aidha majimaji hayo husaidia kuzipa mbegu za kiume nguvu ya kusafiri kwenye uke mpaka kufikia kwenye mirija ya fallopian tayari kwa utungisho na yai la kike. Vilevile husaidia kupunguza hali ya kitindikali (acidic condition)  iliyopo katika uke, ambayo kama isiporekebishwa, huweza kuua mbegu nyingi za kiume na kufanya utungisho kuwa wa shida.

Kwa kadiri mwanaume anavyozeeka, ni jambo la kawaida pia kwa tezi dume kuongezeka ukubwa na kuvimba. Hali hii kitabibu huitwa Benign Prostate Hyperplasia au wengine hupenda kutumia maneno Benign Prostate Hypertrophy kwa kifupi BPH. Hivyo tezi inaweza ikawa kubwa sana lakini haina dalili hii ni kutokana na sehemu gani ya tezi iliyovimba au kuongezeka. Tezi inapoonesha dalili jua tatizo hilo ni sugu na liko ktk hali mbaya. Kwenye makala hii tutautumia sana ufupisho huu wa BPH ili kurahisisha kuelewa.
Ukuaji wa tezi dume hupitia hatua kuu mbili. Hatua ya kwanza hutokea kipindi cha balehe wakati tezi dume linapoongezeka ukubwa na kuwa mara mbili ya lilivyokuwa hapo awali. Baada ya hapo ukuaji husimama kwa muda mpaka kijana anapofikisha miaka 25 hadi 30 ndipo hatua ya pili ya ukuaji huanza tena. Ukuaji huendelea kwa viwango na kasi tofauti kati ya mtu na mtu na hatimaye kusababisha BPH katika umri wa utu uzima.
Wakati tezi dume linapokua na kutanuka, utando wa tishu unaozulizunguka hutanuka pia. Hata hivyo ingawa tezi dume huendelea kukua, hufikia wakati utando wake huacha kutanuka na kufanya tezi dume kubana mrija wa kutolea mkojo kutoka kwenye kibofu. Hali hii husababisha kibofu cha mkojo kuwa na ngozi ngumu. Hali hii hufanya kibofu cha mkojo kuhisi kutaka kutoa mkojo nje hata kama kiasi cha mkojo ndani yake ni kidogo sana. Hufikia wakati, kibofu huwa dhaifu na kupoteza uwezo wake wa kuhisi kutoa mkojo na hivyo kufanya mtu anapokojoa kushindwa kutoa mkojo wote na badala yake hubakiza kiasi fulani cha mkojo kwenye kibofu.
Bph (Kuvimba tezi dume) Husababishwa na nini?


Chanzo halisi cha BPH au vihatarishi vyake (risk factors) havijulikani kwa uhakika. Kwa muda mrefu imekuwa ikichukuliwa kuwa BPH hutokea kwa wanaume watu wazima na wazee tu. Aidha imewahi kuonekana huko nyuma kuwa PBH haitokei kwa wanaume ambao wamewahi kufanyiwa operesheni ya kuondoa korodani au wale ambao walizaliwa bila korodani. Hali imepelekea baadhi ya watafiti kuamini kuwa BPH ina uhusiano mkubwa na umri wa mtu pamoja na uwepo wa korodani.
Dhana  kadhaa zinazojaribu kuelezea chanzo cha BPH. Dhana hizo ni pamoja na
·           Uhusiano kati ya BPH na homoni ya estrogen: Wanaume huzalisha testosterone, homoni ya muhimu sana katika mwili wa mwanaume. Hali kadhalika huzalisha pia estrogen ambayo ni homoni ya kike kwa kiwango kidogo sana. Kadiri jinsi mtu anavyozeeka, ndivyo uzalishaji wa testosterone unavyokuwa mdogo na kufanya kiwango chake katika damu kupungua kulinganisha na kiwango cha estrogen ambacho huongezeka kwa kiasi fulani. Pamoja na kazi nyingine, estrogen pia huchochea ukuaji wa chembe hai za mwili. Tafiti zilizofanywa kwa wanyama zimeonesha kuwa BPH hutokea kwa sababu kiwango kikubwa cha estrogen katika damu huchochea ukuaji wa seli za tezi dume na hivyo kufanya tezi dume kuvimba.
·           Uhusiano kati ya BPH na Dihydrotestosterone (DHT):                 DHT ni kiasili kinachozalishwa kutokana na testosterone kwenye tezi dume, ambacho husaidia kuthibiti ukuaji wa tezi dume. Ingawa wanyama wengi hupoteza uwezo wa kuzalisha DHT wanapofikia umri wa uzee, baadhi ya tafiti zimeonesha kuwa, kwa binadamu, hata kama kiwango cha testosterone kitapungua sana katika damu, wanaume watu wazima bado wana uwezo wa kuzalisha kiasili hiki cha DHT katika tezi dume zao. Uzalishaji huu wa DHT huchochea kwa kiasi kikubwa ukuaji wa seli za tezi dume na kusababisha BPH. Wanasayansi wamegundua kuwa wanaume watu wazima wenye kiwango kidogo cha DHT hawapati BPH.
·           Uhusiano kati ya BPH na maelekezo ya seli.                                       Dhana nyingine inasema kwamba baadhi ya seli kutoka katika sehemu fulani ya matezi yanayohusika na ukuaji mwilini hupewa maelekezo wakati mtu anapokuwa bado mdogo. Seli hizi hutunza maelekezo hayo na baada ya miaka kadhaa maelekezo haya huanzwa kutekelezwa na seli za matezi mengine. Mojawapo ya melekezo hayo ni kuchochea ukuaji wa tezi dume na kusababisha BPH.
Dalili za kuvimba kwa tezi Dume
1.        Kukojoa mara kwa mara
2.        Kubakiza mkojo kwenye kibofu
3.        Kukujoa sana usiku
4.        Maumivu wakati wa kukojoa
5.        Kupungukiwa nguvu za kiume
6.        UTI ya mara kwa mara
7.        Mawe kwenye kibofu kutokana na mrundikano wa mkojo.
8.        Figo kujaa maji. Hii sababu mkojo huo unarudi nyuma kuelekea figo (hydronephrosis)
9.        Kupoteza fahamu(uremia)
Madhara ya Bph (Kuvimba tezi dume)
BPH kama ilivyo saratani ya tezi dume, inaweza kumletea mgonjwa madhara (complications) kadhaa. Madhara hayo ni pamoja na
·           Mkojo kushindwa kutoka (retention of urine)
·           Mgandamizo kwenye kibofu cha mkojo
·           Vijiwe kwenye kibofu cha mkojo
·           Uambukizi katika njia ya mkojo (UTI)
·           Madhara katika figo au kibofu
·           Shinikizo la damu
·           Kushindwa kutoa shahawa kwenye uume (retrograde ejaculation)
·           Nimonia (Pneumonia)
·           Damu kuganda
Baada ya mgonjwa kujihisi dalili zilizotajwa hapo juu, daktari atamfanyia uchunguzi wa mwili kabla ya kumfanyia vipimo zaidi. Vipimo vyaweza kutofautiana kati ya mgonjwa namgonjwa, lakini baadhi ya vipimo ni pamoja na
1.KUCHUNGUZA TEZI DUME KUPITIA NJIA YA HAJA KUBWA AU DIGITAL RECTAL EXAMINATION (DRE)

Hiki ni kipimo cha kwanza kabisa ambacho mgonjwa hufanyiwa na daktari wake. Ni kipimo kinachoweza kumpa daktari picha ya tatizo na kufahamu kuhusu ukubwa na hali ya tezi dume. Daktari akiwa amevaa glovu huingiza kidole chake cha shahada katika njia ya haja kubwa au puru (rectum) ya mgonjwa kasha kuzungusha zungusha ili kufahamu kama tezi limevimba ama la na pia hali yake kama ni gumu kuliko kawaida ama lina utando na nyama laini.
2.KIPIMO CHA DAMU CHA PROSTATE-SPECIFIC ANTIGEN (PSA):
PSA husaidia kutofautisha kati ya saratani ya tezi dume na BPH. PSA ni aina ya protein inayozalishwa na seli za tezi dume na kiwango chake huongezeka iwapo kuna saratani ya tezi dume.
3.UTRASOUND YA PURU (RECTAL ULTRASOUND)
Kipimo hiki hufanyika iwapo daktari atahisi kuwepo kwa saratani ya tezi dume badala ya BPH. Utrasound ya puru pamoja na kuonesha taswira ya tezi dume ilivyo, pia humuwezesha daktari kuchukua kinyama (biopsy) kwenye tezi dume kwa ajili ya uchunguzi zaidi ili kutofautisha kati ya saratani na BPH.
4.KIWANGO CHA UTOKAJI WA MKOJO (URINE FLOW STUDY):Ni kipimo kinachotumika kufahamu kasi ya utokaji wa mkojo. Mkojo unaotoka kwa kasi na kiwango kidogo huashiria kuwepo kwa BPH.
5.        KIPIMO CHA KUCHUNGUZA KIBOFU CHA MKOJO (CYSTOSCOPY): Kipimo hiki husaidia kuweza kufahamu ukubwa wa tezi, sehemu tezi lilipobana njia ya mkojo na kiwango cha kubana huko. Aidha huwezesha pia kutambua hali ya kibofu cha mkojo ikoje.
Matibabu ya tezi dume.

Matibabu ya BPH yameganyika katika sehemu mbili, yale yanayofanywa kwa kutumia dawa na yale yanayofanywa kwa kutumia upasuaji mdogo. Aidha matibabu hufanywa kwa watu wenye BPH kubwa zaidi na dalili zinazowaletea usumbufu na kuathiri maisha yao, wakati wale wenye dalili ndogo ndogo hawalazimiki sana kuhitaji matibabu.
Matibabu kwa njia ya dawa
Dawa hizi hutumika kwa lengo la kulifanya tezi dume kusinyaa na kupungua ukubwa wake.
Matibabu kwa njia ya upasuaji
·           Upasuaji mdogo husaidia kuondoa dalili za BPH na hufanyika pale ambapo matibabu kwa njia ya dawa yameshindwa kuonesha mafanikio yeyote. Njia hizo niTiba ya kutumia mawimbi ya joto (Transurethral microwave procedures, TUMT): Tiba hii hutumia kifaa kinachotoa mawimbi ya joto (microwave) yanayochoma na kuharibu tishu zilizovimba za tezi dume.
·           Matibabu huchukua chini ya saa moja na yanaweza kufanyika bila mgonjwa kuhitaji kulazwa.Tiba ya kutumia sindano maalum (Transurethral needle ablation, TUNA): Njia hii hutumia visindano vidogo ambavyo huunganiswa kwenye chombo chenye kutoa nishati ya joto kuunguza tishu zilizovimba za tezi dume.
Tiba ya kutumia joto la maji (Water-induced thermotherapy): Tiba hii hutumia maji ya moto yaliyochemshwa kwa kifaa maalum kuunguza na kupunguza tishu zilizovimba za tezi dume.
Madaktari wengi hushauri kuondolewa kabisa kwa tezi dume iwapo itathibitika kuwa mgonjwa ana BPH. Zipo njia nyingi za upasuaji wa BPH, nazo ni pamoja na upasuaji kwa kupitia kwenye mrija wa mkojo (Transurethral surgery, TURP), upasuaji mkubwa wa wazi (Open surgery), upasuaji wa kutumia nishati kuondoa tishu za tezi dume Laser surgery), na upasuaji wa kutumia joto la fibreoptic probe kuchoma tishu za tezi dume (Interstitial laser coagulation).


Hilo ndio tezi dume tusiyafuge.

No comments:

Post a Comment

Pages