KUWA TAJIRI UKIWA BADO KIJANA - waleo blog

Breaking

Wednesday 19 February 2020

KUWA TAJIRI UKIWA BADO KIJANA



Safari ya kufikia mafanikio siyo rahisi kama ambavyo wengi wanafikiria. Ni safari ambayo inaweza kuwa ngumu sana hasa pale unapozungukwa na jamii ambayo haioni kile unachokiona wewe.
Ili kufikia mafanikio ni muhimu sana wewe kuweka malengo na mipango yako mapema kisha kuifanyia kazi bila kukata tamaa hata kama mambo yatakuwa magumu kiasi gani.

Sisi sote tunataka na kutamani kuwa matajiri. Kwa wengi wetu, ni ndoto  tangu utotoni kwamba siku moja tutakuwa matajiri. Ukweli ni kwamba, pamoja na kuwa ni kazi ngumu, lakini tukiamua, tunaweza kujitengeneza sisi wenyewe kuwa mamilionea au mabilionea.
Lakini ukweli ni kwamba, kuwa tajiri siyo jambo la siku moja, yaani kuamka na kujikuta wewe ni tajiri. Pia ni vigumu sana unapofikia uzee ndiyo uanze kutafuta utajiri. Jambo hili huanza tangu mtu akiwa mdogo, akiwa na uwezo wa kuunganisha bahati na nguvu zake za mwili na akili.

Zipo tafiti nyingi zinazoonesha kuwa, umri mzuri na usiokuwa na changamoto nyingi za kujijenga kufikia utajiri mkubwa ni katika kipindi cha miaka 20 hadi 30.
Huenda kipindi hiki ukawa ni mwanafunzi na ukawa na changamoto nyingi za kimasomo ambazo zitakuzuia kufanya kitu kingine nje ya masomo kwa hofu ya kukosa vyote.

Lakini kumbuka, hakuna njia ya moja kwa moja ya kujihakikishia kuwa tajiri baadaye. Hapa ndipo linapokuja suala la kupata elimu sahihi ya unachokitaka kisha linakuja suala la kupanga ni kuchagua na kwa wale wenye uwezo mkubwa wa kiakili, wanaweza kuhimili yote kwa wakati mmoja. Yaani kusoma na wakati huohuo kufanya biashara hata kama ni ndogondogo. Mtu huyu anaweza kuanza na ‘vibiashara’ ambavyo wenzake watamwambia kuwa anapoteza muda bila kujua anatengeneza mazingira ya kupata uzoefu wa kwenda kukabiliana na maisha hasa atakapomaliza masomo na kukutana na tatizo kubwa la ajira.
Hapa nitajaribu kukupa njia saba (7) ambazo zaweza kukusaidia kukujenga na kufikia utajiri mkubwa tangu ukiwa na umri mdogo wa kati ya miaka 20 hadi 30;


1: Amini huna muda mwingine

Unapokuwa na umri huo na ndoto yako ikawa ni siku moja kuwa tajiri, anza mapema. Ujinga wa vijana wengi ni kuamini kuwa daima kuna muda wa kutosha kwa kila kitu hivyo atafanya tu!
Vijana mara nyingi wanaamini kwamba kuanza biashara mapema au kujenga ni mambo yanayokuja baadaye hivyo hujipumbaza kwa kuona kuwa bado muda upo.
Kwa hiyo, kwa mantiki hii, hatua ya kwanza ni kuacha kusubiri muda fulani ufike maana hautafika. Wengine wanakuwa tayari kuwekeza, lakini wanaogopa suala la umri.

2: Hakuna uchawi


Matumizi ya neno ‘njia’ kwenye kichwa cha mada hii ni kukuondoa kwenye mambo ya gizani. Nilitamani kutumia neno ‘siri’, lakini nikaliacha ili mtu asiamini kwamba kuwa tajiri kuna nguvu za giza.
Hapa hakuna uchawi, ninachokufundisha ni ufumbuzi wa uhakika wa kukufanya tajiri. Uchawi pekee ni kutumia kidogo unachopewa na mzazi au mlezi na kuanza kufanya ujasiriamali hata kama ni wa shilingi elfu kumi wakati bado ukiwa masomoni.
Katika mazingira kama hayo, jinsi unavyowekeza ni juu yako kutokana na kile unachokipata kwa mjomba au shangazi anapokuaga wakati unapochaguliwa kujiunga na ngazi fulani ya elimu.

Rafiki yangu usikubali kutumia chote unachopewa au kukipata hadi kikaisha chote bila hata kuanzisha mradi wa kuuza mafuta ya taa mtaani au maandazi kijijini au mtaani kwenu kupitia ndugu, rafiki au jamaa ambaye utamwamini ambaye hakupata nafasi ya kuendelea na masomo au aliyemaliza masomo awe msimamizi wako. Hapa usiwaze sana kuibiwa au kudhulumiwa kwani hilo laweza kukutokea hata ukiwa unasimamia mwenyewe.

3: Kuwekeza ndani yako

Baada ya kujua kuwa, huna muda na hakuna uchawi katika mambo haya, njia ya tatu ni kuanza mapema kadiri iwezekanavyo kuwekeza ndani yako.
Jambo moja muhimu wasilolijua wengi ni kwamba wewe ni rasilimali kubwa ya kujitengenezea utajiri. Kuwekeza ndani yako wewe mwenyewe inamaanisha kutumia muda wako mwingi zaidi kujijenga mno katika kupata ujuzi na kujiunganisha na watu unaoamini wanaweza kukufikisha kwenye ndoto yako ya kuwa tajiri.
Kwa wale waliopata bahati ya kwenda shule, wenye ujuzi na uzoefu katika eneo fulani, wana fursa kubwa sana wanayoipata na kuwarahisishia njia zao.

4: Panga bajeti

Kama nilivyosema awali, unaweza ukapata pesa kiasi fulani. Pesa hiyo ni lazima iwe na bajeti la sivyo hutajua imepitia wapi, kufumba na kufumbua utakuta huna hata kumi. Tumia kidogo na nyingine fanya uwekezaji. Panga bajeti ya kina juu ya chochote unachokipata. Weka mipaka imara kwa gharama zako ukizingatia pesa zikija huwa zinakutekenya ili uzitoe ziondoke zake.

5: Epuka madeni

Kabla ya kuanza kutafuta na kuwekeza pesa, ni lazima ujilinde na madeni ambayo yaweza kukutoa kwenye reli. Ukiacha mikopo ya masomo, ogopa sana mikopo ya magari na vitu visivyokuwa vya lazima kwenye umri huo. Rafiki, ukishatengeneza pesa, magari siyo ishu maana utaendesha ya kila aina, tena yenye majina makubwa.

6: Usiogope kupoteza

Katika umri huo mdogo, usiogope kupoteza kwani unakuwa na miaka mingi mbele yako kama Mungu atakujalia uhai. Usiogope kuwekeza kwenye maeneo hatarishi zaidi. Fikiria, ukimaliza masomo, usiwaze kuajiriwa, anza biashara yako mwenyewe. Vijana wengi wanaamini kwamba, ajira ndiyo ulinzi na usalama wa maisha yao, lakini kwako iwe tofauti kwani nilishaeleza ulemavu wa kuajiriwa uliyo mbaya.

7: Usitegemee ujuzi wa aina moja

Kuthubutu katika uwekezaji hata kama ni wa shilingi kumi ndiyo msingi wa kuanza kufanya jambo. Lakini nakukumbusha tu kuwa, usitegemee ujuzi wa aina moja. Jichanganye kwa kujiongeza kujua ujuzi mwingine na mwingine. Pia usitegemee aina moja tu ya uwekezaji, badala yake jaribu kuanzisha vyanzo vingi vya mapato, uzalishe mipangilio kadhaa ya uhifadhi kwa malengo na biashara zako, tafuta fursa mpya kila mahali na kila kukicha.


Ninaamini kuwa, kwa kutumia njia hizi saba na Mungu akikujalia uzima, utakuwa na uwezo wa kuanza kutengeneza utajiri bila kujali mahali ulipo.

No comments:

Post a Comment

Pages