ASILI YA MUZIKI NCHINI TANZANIA. - waleo blog

Breaking

Wednesday 25 March 2020

ASILI YA MUZIKI NCHINI TANZANIA.


#Burudani

Muziki wa Tanzania ni jina la muziki wenye asili ya Tanzania ya leo. Kama ilivyokuwa kwa binadamu wengine, wakazi wa eneo ambalo limekuwa nchi ya Tanzania, walikuwa na utamaduni wao. Utamaduni huu ulikuwa ukitofautiana kati ya kabila na kabila. Moja ya vipengele ilikuwa muziki. Kiasili, hatukuwa na muziki katika makabila yetu kabla ya ujio wa wageni, na hivyo hakuna kabila lenye tafsiri ya neno muziki.
Lakini tuliimba, tulicheza ngoma, tulipiga vyombo mbalimbali, ila tulikuwa na utamaduni mwingine kuhusu kitu hiki tunachokiita siku hizi muziki. Watafiti wanatuambia tulikuwa na ngoma, ambayo tafsiri yake ni kubwa kuliko muziki.
Ngoma ilikuwa ni chombo kile kilichotoa muziki, ngoma ilikuwa shughuli yenyewe, kwa mfano ngoma ya mavuno, ngoma ya mashetani na kadhalika, na pia tulicheza ngoma. Pamoja na kukosekana kwa maandiko yenye kina kuhusu hali ya ngoma katika kipindi hicho lakini tunajua watu waliimba na kucheza ngoma kwa matukio mbalimbali, hali ambayo inaendelea mpaka leo.

Wajerumani ndio waliotuletea neno muziki, na katika wakati wao wa utawala ndipo kuliingia muziki wa bendi za askari na kuingizwa katika shule ya kwanza ya serikali wakati huo na Tanga School ni moja wapo. Katika kipindi hiki pia mchango wa madhehebu mbalimbali kuingiza muziki na vyombo vya muziki vipya ulitoa mchango katika kuongeza kasi ya huu muziki mpya.
Pengine unaweza ukasema kuwa, kipindi hiki kwaya nazo zilianza kushika kasi, hapa unaona kama neno kwaya pia ni jipya lililotokana na neno la Kiingereza choir. Historia inatueleza kuwa Mjerumani hakufanya jitihada za kuzuia muziki wa kiasili, hivyo basi muziki mpya na wa kiasili ulienda sambamba.

Mwingereza alileta mabadiliko mengi katika muziki wanchi hii. Askari waliotoka vitani KAR maarufu kama askari kea walirudi na hadithi kuhusu muziki, vyombo vya muziki, na hata muziki walioukuta katika safari zao vitani, vyombo kama akodian na magitaa makavu yaani, yasiyotumia umeme yaliingia wakati huu. Kutokana na watu wa makabila mbalimbali kuchanganyika na miji kuanza kuzaliwa kukaanza kuweko na utamaduni mpya.
Muziki uliyokuwa unakubalika kwa makabila yote ulianza. Aina ya muziki maarufu kama Beni ilienea katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki. Waafrika waliokuwa wamesoma nao wakaanza kuwaiga Wazungu hata kuanza kuteengeneza Club zao ambazo zilikuwa maarufu kama Dancing Clubs. Katika club hizi kulipigwa nyimbo mbalimbali kwa kutumia santuri na wapenzi kucheza muziki katika staili mbalimbali kama vile Cha cha, Tango, Foxtrot, swing, waltz n.k.
Inasemekana clabu ya kwanza Tanzanyika ilianza Tanga, ikiitwa Young Noverty Dancing Club, na baadaye Dar es Salaam ikawa na Young Generation Dancing Club. Club hizi zilikuwa ndio chanzo cha bendi za kwanza Dar es Salaam Social Orchestra ambayo baadaye ilikuja kuwa bendi maarufu Dar es Salaam Jazz Band, na pia kulikuweko na YMCA Social Orchestra, wakati huu ilikuwa katika kipindi cha kati ya 1920 na 1935. Baada ya vita ya pili ya dunia 1945Wamarekani waliweka radio yenye nguvu katika mji unaoitwa sasa Kinshasa, redio hii iliweza kusikika sehemu nyingi, Afrika mashariki, Kati na Magharibi. Kuanza kwa lebo maarufu ya Loningisa nchini Kongo mwaka 1947 ilianzisha kusikika na kuigwa kwa muziki wa Kikongo kuanzia wakati huo.
Lebo ya Galotone ya Afrika Kusini pia ilisambaza santuri ambazo ziliingiza staili za Jive katika nchi hii na kwa miaka mingi vijana walikuwa na vikundi wakicheza jive, na bendi kadhaa ziliiga upigaji wa jive ukiambatana na upigaji wa filimbi kumuiga mwanamuziki Spokes Mashiyane. Magitaa ya umeme kwa bendi za muziki wa dansi yalianza kutumiwa kati ya mwaka 1957 na 1959, Dar Jazz tena hutajwa kama bendi ya kwanza ya muziki wa dansi kuanza kutumia gitaa hilo, ikifuatiwa na Western Jazz na bendi nyinginezo.
Kwenye mwaka 1954 Kenya ikaanza kuwa kituo kikubwa cha kurekodi muziki, na kwa miaka mingi iliyofuata bendi za Afrika Mashariki zililazimika kwenda Kenya ili kutoa santuri. Kuna wanamuziki wengine mpaka leo hufikiriwa ni Wakenya au nyimbo zao kudhaniwa kuwa zilitoka Kenya kwa mfano Frank Humplink na dada zake ambao walitoa vibao ambavyo bado vinasikika katika anga za muziki hadi leo, embe dodo, tufurahi tarusi n.k

Pamoja na mapungufu yanayotajwa ya utawala wa chama kimoja, kulikuweko na mambo yaliyowezekana kutokana na hali ya chama kimoja kuwa na dira inayoeleweka na hivyo kuelekeza kila kitu kadri ya matakwa ya chama. Sanaa ya Tanzania haikukwepa mwongozo wa TANU, sehemu za kazi , vijiji , miji viliagizwa kuwa na vikundi vya utamaduni ambavyo vingekuwa ndio vikundi vya burudani baada ya kazi na pia jukwaa la kuelezea mipango na malengo ya chama na serikali. Zikatengenezwa bendi za majeshi, polisi, JWTZ, Magereza, Uhamiaji, mashirika ya umma nayo hayakuwa nyumaBIMATANCUTDDC MlimaniUDA na miji nayo ikawa na bendi Kurugenzi Arusha Kurugenzi Dodoma. Na ni ukweli usiopingika nyimbo nyingi maarufu kama zilipendwa zilipatikana katika kipindi hiki.

Bendi zilitunga nyimbo, ambazo zilipitia katika kamati iliyozipitia kabla ya kuruhusiwa kurekodiwa na kurushwa hewani. Kwa upande wake serikali nayo ikatengeneza idhaa/chanel tatu katika redio ya taifa, External Service, iliyokuwa ikitangaza kwa lugha ya Kiingereza na lugha ya nchi za kusini zilizokuwa zikipigania uhuru wakati huo, kukaweko na Idhaa ya biashara ambayo ilikuwa na vipindi vikitangaza biashara mbalimbali vilivyodhaminiwa na wafanya biashara. Katika idhaa hii, uliweza kusikia muziki kutoka popote duniani, lakini kwa makusudi kabisa kukaweko na idhaa ya taifa ambako huku ungesikia kila aina ya muziki wanchi hii, pamoja na kuwa kwa sasa kuna vituo vya radio zaidi ya 80 vimeshindwa kufanya kazi hii iliyoweza kufanywa na kituo kimoja cha taifa.Ubaya ulioje,  kituo hicho cha taifa kimeshapoteza muelekeo wake uliokuweko awali.
Katika miaka ya mwanzoni ya 1960, bendi ziliingia katika utamaduni wa kunakili nyimbo kutoka Kongo na kuimba Kiswahili tu. Kuna nyimbo kama napenda nipate lau nafasi, mtoto wacha kupiga mayowe na nyingi sana ambazo zilikuwa ni za kunakili moja kwa moja nyimbo za Kongo. Hali ilifikia kuwa mbaya mpaka bendi nyingine ziliingilia kati na kutunga nyimbo za kuwaasa wenzao watunge nyimbo zao.mfano;Koma koma koma kaka wewe tunga zako. ilikuwa baadhi ya maneno ya kuwafanya wanamuziki waliokuwa wakiiga waache kuiga.
Lakini pamoja na haya kulikuweko na wanamuziki waliokuwa wakiangalia na kuiga nyayo kutoka nchi za magharibi na baadaye wakichanganya vyombo na melodi za kiasili na kuanza muziki uliojulikana kama Afro Rock, na kuwa sambamba na nchi nyingine katika Afrika. Katika kipindi hiki mwanasiasa mmoja aliwahi kupiga marufuku muziki wa bugi, ambao ulikuwa ni maonyesho ya muziki ya mchana yaliyokuwa yakisha saa kumi na mbili, na kwa kupiga marufuku muziki huo ilikuwa ni sawa na leo upige marufuku wanamuziki wa kizazi kipya. Pengo aliloliweka halijaweza kujazwa tena.
Katika miaka ya 1980/1990
Katika kipindi hiki kulikuweko na mfumo wa utawala wa shughuli za Utamaduni ambao pamoja na kuweko maafisa utamaduni wa wilaya, maafisa utamaduni wa mikoa , pia kulikuweko na baraza la muziki la taifa (BAMUTA).Kulizaliwa vyama ambavyo vilifanya kazi kubwa katika kuunganisha wanamuziki kama vile CHAMUDATA na Tanzania Taarab Association. Na itakuwa ni makosa kutotaja show iliyokuwa kubwa sana na iliyounganisha wanamuziki wa nchi nzima TOP TEN Show.
Show hii iliyowezekana kwa ushirikiano wa BASATAumoja wa vijanaradio Tanzania na halijawahi kutokea tena onyesho lenye ukubwa wa aina hiyo mpaka leo. Kuvurugika kwa mfumo wa uongozi wa utamaduni kwa kuwaondoa maafisa utamaduni walioko chini ya wizara ya utamaduni umeacha shughuli za utamaduni mkononi mwa wafanyabiashara pekee, ambao kwao lengo ni kupata faida za kiuchumi.Matatizo na matokeo ya kufa kwa utamaduni si lolote kwao. Serikali inatakiwa ichukue mzigo huu wa kufadhili ukuaji na uendelezaji wa utamaduni, na kuacha shughuli za biashara ya kazi za sanaa kwa wafanya biashara.
Zama hizi ndizo zilizozaa muziki wa kizazi kipya maarufu kama Bongo flava. Zama hizi kuna mapinduzi makubwa sana katika muziki nchini Tanzania.Bendi nyingi za muziki wa dansi zilianzishwa, hasa kwa wale wakongwe na kuunda bendi zao binafsi. Kukua kwa teknolojia na kuanza matumizi ya tarakilishi/kompyuta katika utayarishaji wa muziki. Hapa hasa vijana ndipo waliposhika hatamu na muziki wa kizazi kipya. Ottu Jazz Band miaka hii walitumia mtindo wa "Discipline" na walitingisha hasa katika miaka hii. Miaka hii ndipo palipoanza kuwa na taasisi au kampuni kubwa za uburudishaji wa muziki kama vile Radio One, Clouds FM, Radio Uhuru, Times FM na nyingine nyingi tu.
Sehemu kubwa ya vijana waliozaliwa miaka ya 1980 na 1990 mwanzoni walianza hamasa ya kutaka kuwa wanamuziki na kujishughulisha na kazi za muziki kwa kiasi kikubwa sana. Kipindi hiki ndiko kulikotokea makundi mbalimbali ya muziki wa hip hop ikiwa ni pamoja na Gangwe MobbDewplomatzS.O.S B., Kwanza UnitUnderground SoulzHard Blasterz, na wengine wengi tu. Kipindi hiki ndicho alipoibuka Saleh Jabri anayesemekana kuanzisha muziki wa hip hop kwa kiswahili nchini Tanzania. Moja ya kazi za Saleh ni ile aliyorudia wimbo wa Vanilla Ice "Ice Ice Baby" kwa kutia maneno ya Kiswahili.
Katika miaka ya 2000/2010
Katika kipindi hiki, muziki uliokuja juu sana ulikuwa "Bongo Flava na muziki wa dansi ambao hasa vijana wapya au wa muda kiasi walirudi kwa kasi katika kipindi hiki. Hapa bendi ambazo zilijaribu katika kipindi cha miaka ya 1990 katikakati na mwishoni zilirudi na zilivuma kupita kiasi. Bendi kama African Revolution iliyokuwa inatumia jina au mtindo wa chumvi-chumvi tutalamba ilirudi na jina la "Tam-tam" chini ya uongozi wake kocha wa dunia Mwinjuma Muumini. Vilevile T.O.T Plus Band, The African Stars, akina Bob Rudala, Jungle Survivors Band na nyimbo yao ya Maprosoo, Malaika Band, Extra Bongo, Double M Sound ya Mwinjuma Muumin, Mchinga Sound, Diamond Sound, Akudo Impact, Inafrica Band na bendi nyinginezo nyingi zilitingisha katika zama hizi. Chuchu Sound Band ni miongoni mwa bendi zilizotamba sana mwanzoni mwa miaka ya 2000. Waliimba mtindo wa chakacha au mduara kwa lugha maarufu. Bendi hii ilikuwa tishio katika mtindo huo. Bila kuisahau Kilimanjaro Connection Band.    Itaendelea

No comments:

Post a Comment

Pages