MAZOEZI MEPESI KIAFYA NA FAIDA ZAKE - waleo blog

Breaking

Thursday 19 December 2019

MAZOEZI MEPESI KIAFYA NA FAIDA ZAKE

#AFYA

Kwa mujibu wa Shirika la Afya la duniani (WHO) ili kuwa na afya njema na kujenga mwili imara,unahitajika kufanya mazoezi mepesi angalau kwa dakika 150 kwa wiki yaani kwa siku dakika 30 katika siku tano za wiki.
Muda huo ndiyo unatupa faida za kiafya zifuatazo ambazo unaweza kuzipata endapo utayafanya mazoezi haya kwa ratiba.
1.Kukukinga na magonjwa
Kupunguza hatari ya kupata magonjwa yasiyoambukiza ikiwamo magonjwa ya moyo, kiharusi, saratani na kisukari kwa sababu mazoezi yanasaidia kuwa na mfumo wa moyo na damu yenye afya njema.
2. Kudhibiti unene
Unene ni kihatarishi cha kupata magonjwa mbalimbali yasiyoambukiza, kufanya mazoezi kunashughulisha viungo vya mwili hivyo kuchoma mafuta yaliyorundikana hatimaye kudhibiti uzito uliokithiri.
3. Kushusha shinikizo
Mazoezi yanasababisha kuwa na moyo na mishipa ya damu yenye afya njema kuchangia kushusha shinikizo la juu la damu ambalo ni sawa na tendo la uuaji wa kimyakimya.
4. Mfumo wa hewa
Kufanya mazoezi kama kutembea, kukimbia na kuogelea kunasaidia misuli ya mwili kuwa na ufanisi wa juu kusafirisha na kutumia oksijeni katika mapafu pamoja na kutoa hewa chafu nje ya mwili.
5. Mfumo wa chakula
Mazoezi yanakufanya kuwa na hamu ya chakula na maji, husaidia chakula kusagwa, kunyonywa na kutolewa kwa ufanisi mwilini na kukuepusha na tatizo gesi na ukosefu wa haja kubwa.
6. Kupunguza hatari ya kupata saratani
Tafiti zinaonyesha wanaofanya mazoezi huondokana na hatari ya kupata saratani za ziwa, utumbo mpana na mapafu ukiwalinganisha na wasiofanya.
7. Kudhibiti lehemu mbaya
Lehemu (cholesterol) ni mafuta ndani ya mishipa ya damu, mazoezi yanapunguza kiwango cha lehemu mbaya na kuongeza kiwango cha lehemu nzuri ambayo ina faida mwilini.
Lehemu mbaya ndiyo inaharibu mishipa ya damu ikiwamo ya moyo, hivyo kuidhibiti hupunguza hatari ya shambulizi la moyo (heart attack) na kiharusi (stroke).
8. Kinga imara
Kadiri unavyofanya mazoezi mara kwa mara ndivyo hatari ya kuumwa na magonjwa mbalimbali inavyopungua hii ni kutokana na mazoezi kukufanya kuwa na kinga madhubuti dhidi ya vimelea.
9. Misuli imara
Kuimarisha misuli na kukupa ukakamavu wa mwili kwasababu mazoezi yanaifanya misuli kujengeka na kudumu, hivyo kuweza kukabiliana na mazingira magumu.
10. Maungio mepesi
Kusaidia maungio na viungo vya mwili kuwa myepesi hivyo kufanya matendo mbalimbali ya kimwili kwa haraka na ufanisi pasipo kupata majeraha kirahisi.
11. Mifupa imara
Kusaidia kuwa na mifupa imara iliyojengeneka, hivyo kupunguza hatari ya kupata tatizo la kumomonyoka mifupa lijulikanalo kitabibu kama Osteoporosis.
13. Usingizi mnono
Kuchangia kupata utulivu kimwili, hivyo kupata usingizi mnono. Usingizi una faida kwa mwili ikiwamo kusahihisha hitilafu mbalimbali za mwilini na kujenga kinga imara na mwili
14. Kuboresha afya ya akili
Kemikali ijulikanayo kama Endophins inayozalishwa wakati wa ufanyaji wa mazoezi husababisha mwili kupata hisia nzuri ikiwamo furaha.
Vilevile mazoezi humsaidia mtu kupeperusha hisia hasi ikiwamo hofu, woga, sonona (depression) na kumfanya ajihisi ni mtu mpya.
15.Mienendo
Kujenga utegemezi na mazoezi na kuyazoea sana husaidia kushikamana nayo, hivyo kukuepusha na vishawishi ikiwamo mienendo na mitindo mibaya kama vile utumiaji tumbaku, ulaji holela wa vyakula, ulevi na uasherati.
16. Kuondoa sumu
Wakati wa mazoezi jasho hutoka kwa wingi pamoja taka sumu na maji ambayo hutoka pamoja na joto lililozidi, hivyo kusaidia kulinda joto la ndani ya mwili.
17. Kuboresha ngozi
Kutoa taka sumu yaani jasho kunaisafisha ngozi na kuifanya kuwa na afya, vilevile misuli iliyotuna huifanya ngozi kuvutika na kuwa ng’avu ndiyo maana wanaofanya mazoezi huonekana wenye afya na wasiozeeka.
18. Hamu ya kunywa maji mengi
Kupata kiu baada ya kutokwa jasho hukufanya kunywa maji kwa wingi. Maji yana faida lukuki kiafya ndiyo maana unaweza kuishi bila chakula lakini si bila maji.
Maji hurudishia maji na chumvichumvi zilizopotea kwa njia ya jasho wakati wa mazoezi, hivyo kukufanya kuendelea kuwa na mzunguko mzuri wa damu.
19. Kuondoa uchovu na maumivu
Uchovu husababisha hisia za mwili kuuma, mazoezi huondoa mrundikano wa tindikali ya Lactic ambayo ndiyo inasababisha uchovu, maumivu na kukakamaa au kuwaka moto kwa misuli. Vilevile kupunguza maumivu wakati wa hedhi kwa wanawake.
20. Tendo la ndoa
Mazoezi huongeza uimara wa misuli ikiwamo ile ya misuli ya kitako cha kiuno ambayo ndiyo inayoongeza ufanisi katika tendo la ndoa kwa pande zote mbili, hivyo kuimarisha uhusiano.
21. Nguvu za kiume
Mazoezi husaidia kuongeza nguvu za kiume kwa kuchochea kuzalishwa kichochezi cha kiume, kudhibiti unene uliokithiri, utiririkaji wa damu katika misuli ya uume na kuondoa woga wakati wa tendo.
22. Uimara na nguvu kwa mjamzito
Mazoezi humsaidia mwanamke mjamzito kuiandaa misuli ya kiuno na nyonga kutanuka vyema ili kuwezesha kujifungua salama. Pia, kumfanya kuwa na ustahimilivu na nguvu za kumsukuma mtoto anapozaliwa.

No comments:

Post a Comment

Pages